Wachimbaji madini Songwe waruhusiwa kuendelea na shughuli zao
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (kulia mbele) na Meneja wa Kiwanda cha chokaa cha Lime Africa kilichopo katika Kata ya Nanyala Wilayani Mbozi Mkoani Songwe, Fredy Msindo (kushoto mbele) pamoja na msafara wakiendelea na ziara katika eneo la kiwanda hicho ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku mbili katika mkoa wa Songwe yenye lengo la kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini.
Meneja wa Kiwanda cha chokaa cha Lime Africa kilichopo katika Kata ya Nanyala Wilayani Mbozi Mkoani Songwe, Fredy Msindo (katikati) akielezea shughuli zinazofanywa na kiwanda hicho kwa Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo .
Kutoka kushoto Afisa Madini Mkazi katika Mkoa wa Mbeya, Sabai Nyansiri, Afisa Madini kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Mbeya, Ndege Bilagi na Afisa Madini anayesimamia wilaya za Songwe na Chunya, Athuman Kwariko wakinukuu maelekezo yaliyokuwa yanatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) katika mkutano wake na wachimbaji wadogo uliofanyika katika kata ya Nanyala wilayani Mbozi.
Sehemu ya wachimbaji wa madini ya chokaa na ujenzi kutoka katika kata ya Nanyala wilayani Mbozi mkoani Songwe, wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa unatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani).
Diwani wa Viti Maalum kutoka Tarafa ya Iyula iliyopo Wilayani Mbozi mkoani Songwe, Messiah Swella akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) katika mkutano huo.
Na Greyson Mwase, Songwe
Naibu Waziri
wa Madini, Stanslaus Nyongo amewataka wachimbaji wa madini wanaoendesha shughuli zao za uchimbaji wa
madini ya chokaa na ujenzi katika kijiji
cha Nanyala kilichopo katika Wilaya ya Mbozi iliyopo mkoani Songwe kuendelea na
shughuli zao wakati wakisubiri suluhu
ya mgogoro baina yao na kiwanda cha
saruji cha Mbeya.
Naibu Waziri
Nyongo aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumza katika mkutano na wachimbaji
wadogo uliofanyika katika kata ya
Nanyala wilayani Mbozi mkoani Songwe ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku
mbili katika mkoa huo yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa
madini.
Katika ziara
yake Nyongo aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya Songwe, John Palingo, Afisa Madini
Mkazi katika Mkoa wa Mbeya, Sabai Nyansiri, Afisa Madini anayesimamia wilaya za
Songwe na Chunya, Athuman Kwariko, Afisa Madini kutoka Ofisi ya Afisa Madini
Mkazi Mkoa wa Mbeya, Ndege Bilagi, vyombo vya ulinzi na usalama vya wilaya
pamoja na waandishi wa habari.
Nyongo
alifafanua kuwa, awali maelekezo yalitolewa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu
Hassan ya kutaka viongozi kutoka katika mikoa ya Mbeya na Songwe kukaa pamoja
na kuhakikisha wanamaliza mgogoro wa ardhi kati ya wakazi wa Songwe na Mbeya na kiwanda cha
kuzalisha saruji nje ya mahakama jambo ambalo linafanyiwa kazi kwa sasa.
Alielekeza
viongozi kutoka katika mikoa husika kuhakikisha wanashughulikia mgogoro wa
ardhi kati ya mikoa miwili na kiwanda cha saruji cha Mbeya kwa wakati huku
wananchi wanaojishughulisha na shughuli za uchimbaji madini wakiendelea na
shughuli zao kama kawaida katika maeneo husika.
Aliendelea
kusema kuwa, jukumu kuu la Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini ni
kuhakikisha wanatoa leseni za uchimbaji wa madini kwa kuzingatia sheria na
kanuni za madini na kusisitiza kuwa leseni ya uchimbaji wa madini ni tofauti
na hati ya ardhi kwa kuwa inahusisha
madini yaliyopo chini ya ardhi.
“Ningependa
ieleweke kuwa, leseni ya madini inampa mtu kibali cha kuchimba madini yaliyopo
chini ya ardhi ambayo ni tofauti na hati ya ardhi, hivyo wachimbaji wa madini
wana haki ya kuendelea na shughuli za uchimbaji wa madini wakati suala la
mgogoro wa ardhi likiendelea kushughulikiwa na mamlaka husika,” alisisitiza
Nyongo.
Akielezea
taratibu za kuchimba madini mara baada ya kupata leseni, Naibu Waziri Nyongo
alisema mara baada ya mchimbaji kupata leseni ya uchimbaji wa madini anatakiwa
kufika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na baadaye kutambulishwa katika Ofisi ya
Kijiji ili kukutanishwa na wananchi na kufanya makubaliano ya ulipaji fidia
kabla ya kuanza shughuli rasmi za uchimbaji wa madini.
Alisisitiza
kuwa, ni lazima wawekezaji wote katika shughuli za uchimbaji wa madini
kuhakikisha kuwa wanajitambulisha na kufanya makubaliano na wananchi kabla ya
kuanza rasmi kwa uchimbaji wa madini ili kuepuka migogoro ya mara kwa mara.
Katika hatua
nyingine, Naibu Waziri Nyongo aliwataka maafisa madini katika mikoa ya Mbeya na
Songwe kuendelea na zoezi la kuainisha maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo wa
madini ikiwa ni pamoja na utoaji wa leseni ili uchimbaji wao uweze kuleta tija
kwenye uchumi wa nchi.
Aidha,
aliongeza kuwa katika maeneo ambayo ni ya hifadhi au vivutio vya utalii leseni
zake zifutwe ili kuhakikisha rasilimali za maliasili zinalindwa na kuongeza
pato kwenye uchumi wa taifa.
Wakati
huohuo Nyongo aliwataka wachimbaji wa madini kuhakikisha kuwa wanalipa kodi
mbalimbali ili fedha hizo ziweze
kutumika katika uboreshaji wa huduma
nyingine za jamii kama vile elimu, afya, miundombunu ya barabara.
Pia, Nyongo
aliwataka wachimbaji wa madini kuorodhesha kodi na tozo mbalimbali ambazo
wanaona ni nyingi na kuziwasilisha katika Wizara ya Madini, ili Wizara iangalie
namna ya kuzipunguza na wapate faida zaidi kwenye uchimbaji wa madini.
Awali
wakizungumza katika nyakati tofauti wachimbaji hao walieleza changamoto mbalimbali
ikiwa ni pamoja na mgogoro wa ardhi baina yao na kiwanda cha saruji cha Mbeya, uharibifu wa
mazingira unaofanywa na baadhi ya
wachimbaji na ukosefu wa maeneo kwa ajili ya uchimbaji wa madini.
No comments: